Tuesday, June 3, 2014

Kariakoo Market Corporation na Habari Mazao Founders

 Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo  Bwana Florens Seiya akisaini Mkataba baina ya Shirika la Masoko ya Kariakoo na Habari Mazao Founders.Mkataba huu wa ushirikano utawezesha sasa KMC kufanya kazi kwa pamoja na Habari Mazao katika kuhakikisha kuwa bei halisi za mazao zinapatikana kwenye Mtandao wa Shirika muda wote na pia Wadau wengine watazipata taarifa hizi kwa njia ya simu zao za mkononi (SMS Solution). Zoezi hili la utiaji saini ulifanyika jana katika Ofisi ya Meneja Mkuu.
 Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo akiupitia Mkataba kwa  mara ya  mwisho  kabla hajausaini jana Ofisini kwake; na aliyeshikilia mikataba ni Mratibu wa Masoko Project kutoka 2SEEDS Network Bi.Monique Galvao ambaye aliiwakilisha Taasisi hiyo.
 Bi.Monique Galvao muwakilishi wa 2SEEDS Network aliyesimama akitoa maelezo ya msingi kuhusiana na Mkataba wa ushirikiano kati ya KMC na Habari Mazao kwa jinsi gani utakavyokuwa na tija kwa Shirika la Masoko ya Kariakoo.Habari Mazao Founders inawaunganisha vijana hawa Christian Mlayi mwenye T-Shirt ya bluu,Kaboda Suguedo mwenye miwani na Bariki mwenye shati nyeusi.
Mjumbe wa Bodi ya Shirika la Masoko ya Kariakoo Bi. Esther Chogero akitia sahihi yake katika Mkataba wa ushirikiano baina Shirika la Masoko ya Kariakoo na Habari Mazao Founders; kwa ajili ya kufanya kazi pamoja katika Mradi wa ukusanyaji na utoaji taarifa za bei  kutoka Soko kuu la Kariakoo kwa njia ya SMS na Website.Hafla hii ya kutiliana saini ilifanyika jana katika Ofisi ya Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko.

Monday, June 2, 2014

Kariakoo Soko Kuu

 Katika picha hapo juu ni Mratibu wa Masoko Project Bi.Monique Galvao na wengine ni Wataalam wa kutengeneza Mifumo ya Kielekroniki kutoka Habari Mazao Team kijana Bariki na mwenzake Kaboda. Hapa walikuwa katika kikao kujadili namna ya kumalizia Project ya Masoko amabapo wao wanahusika katika uundaji wa mfumo saidizi ambao utafanya kazi sambamba na Mfumo mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo(KMC Database System) katika utoaji wa taarifa mbalimbali za bei za mazo yanayouzwa katika Soko Kuu la Kariakoo.Kikao hiki kilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Shirika la Masoko mwishoni mwa wiki iliyopita.
Kutoka kushoto ni Bariki na Kaboda kutoka Habari Mazao Team wakiwa na Bwana Anderson Shaka yeye ni Mkuu wa Kitengo wa ICT katika Shirika la Masoko ya Kariakoo.Wote wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa kikao  kilicholenga kujadili na kuona jinsi Project ya Masoko itakavyomalizika na kuanza kuwanufaisha Wakulima,Wafanyabiashara pamoja na Walaji wa bidhaa zinazouzwa katika Soko Kuu la Kariakoo.

Thursday, May 29, 2014

Kuna nini Kariakoo Sokoni asubuhiiiii?

 Maembeee! karibu upate maembe ya kila aina yanayozalishwa hapahapa nchini kutoka mikoa ya Tanga,Moro na kwingineko! Karibu sanaa! Matunda ya kila aina huuzwa eneo la Shimoni ndani ya Soko Kuu!
Mratibu wa Masoko Project Bi.Monique Galvao wa 2SEEDS Network na Mrs.Romana Lukanga wakiwa katika pozi  la pamoja mara baada ya maelekezo mafupi namna ya kutumia Smartphone wakati wa kutuma bei za mazao kwenye Mfumo wa taarifa wa Shirika la Masoko(KMC Database System) katika ofisi za Shirika la Masoko.

Kariakoo Market Corporation na 2Seeds Network

Katika picha hapo juu ni Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Kariakoo wakiwa pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa 2SEEDS Network hapa nchini Tanzania Bi.Anna mwenye miwani kulia alipowatembelea wafanyabiashara hapo katika eneo la Soko la jumla  maarufu kwa jina la  Shimoni.Mfanyabiashara aliyesimama karibu naye ni Bwana Munguatosha Mtui yeye ni Mfanyabiashara maarufu wa Karoti na Pilipili hoho.
Katika Picha hapo juu ni Wajumbe wa Menejimenti ya Shirika la Masoko wakiongozwa na Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko Bwana Frolens Seiya wa pili kutoka kushoto na wa kwanza kushoto ni Bwana James Meeks ambaye ni Mwenyekiti wa 2Seeds Network toka nchini Marekani. Hapa ni mara baada ya mkutano uliokuwa ukifanya tathimini ya maendeleo ya Mradi wa Masoko;katika mkutano huo Viongozi Wakuu wa  2SEEDS Network walihudhuria kutoka Marekani.Mkutano huo ulifanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Shirika la Masoko.
Mkuu wa Kitengo cha ICT katika Shirika la Masoko ya Kariakoo Bwana Anderson Shaka akiandikisha jina katika kitabu cha Wageni katika Ofisi za Makao  Makuu ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA). Bwana Anderson Shaka aliambatana na Mratibu wa Masoko Project  Bi.Monique Galvao pichani hayupo; walifika katika Ofisi hiyo kurejesha Fomu ya maombi  ya kununua namba maalum (SHORT CODE) kwa ajili ya Shirika la Masoko ya Kariakoo itakayotumika kwa ajili ya kutoa Taarifa za bei halisi za mazao ambayo huuzwa katika Soko Kuu la Kariakoo.

Mtumishi wa TCRA Bwana Lumumba akiwa anachukua  taarifa mhimu kutoka katika Fomu ya maombi iliyowasilishwa kwa ajili hatua za awali za usajili ili kununua ShortCode kwa ajili ya matumizi ya Shirika la Masoko ya Kariakoo.Aliyesimama ni Bwana Anderson Shaka Mkuu wa Kitengo cha ICT kutoka Shirika la Masoko ya Kariakoo Jijini Dar Es Salaamu,ambaye aliambatana na Bi.Monique Galvao Mratibu wa Masoko Project kutoka 2SEEDS Network.

Mkuu wa Kitengo cha ICT katika Shirika la Masoko ya Kariakoo Bwana Anderson Shaka akifafanua jambo kwa moja  ya Viongozi  wakuu  aliyevaa T-Sheti nyeusi wa Shirika lisilokuwa la Kiserikali liitwalo SEEDS Network lenye makao yake makuu nchini Marekani. Viongozi hawa walifika katika Soko Kuu la Kariakoo kukagua maendeleo ya mradi ambao unatekelezwa kwa ushirikiano baina ya Shirika la Masoko ya Kariakoo (SMK) na 2SEEDS Network,wenye lengo lakuwawezesha Wakulima na Wafanyabiashara wa mazao mbalimbali kupata bei halisi za mazao kutoka Soko Kuu la Kariakoo  kwa njia ya Mtandao kupitia Simu zao mkononi.

Tuesday, May 27, 2014

Sample za Maumbo yatakayotumika katika Soko la Wazi

 Katika picha ni "sample" ya maumbo ambayo yanatarajiwa kutumika Sokoni Kariakoo katika Soko la Wazi ambapo kwa sasa hapajaanza kutumiwa na Wafanyabiashara tangu Manispaa ya Ilala walipovamia na kubomoabomoa meza zilizokuwa zinatumiwa na Wafanyabiashara hao mapema mwanzoni mwa mwezi wa Aprili 2014.Waliosimama na kuziangalia ni Afisa Biashara  Bwana Vedastus Valentine mwenye shati la bluu na Mhandisi wa Shirika Bwana Flavian Mlelwa.
Wafanyabiashara watakuwa wanapanga bidhaa zao humu katika Maumbo haya na kuwauzia Wateja, Maumbo haya yanakusudiwa kuanza kutumika katika eneo la Soko la Wazi katika Viwanja vya Shirika la Masoko ya Kariakoo katika siku chache zijazo mara baada ya taratibu zote kukamilika.

Karibuni Kariakoo Soko Kuu-Jijini Dar-Es Salaam

 katika picha hapo juu ni Katibu Muhtasi  katika Ofisi ya Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo Mrs.Grace Kahatano,kama alivyokutwa Ofisini kwake akiendelea na shughuli zake.
 Shirika la Masoko la Kariakoo lina Idara nyingi mabalimbali, katika Picha hapo juu ni Afisa Biashara Bwana Vedastus Valentine aliyekaa na Mtakwimu wa Shirika la Masoko Bwana Henry  Rwejuna wakiwa ofisini wakijadiliana jambo; wote hawa kwa pamoja wapo katika Idara ya Biashara.
Soko Kuu Kariakoo siyo tuu huuza vyakula pekee bali  ndani ya Soko hili kuna maduka mengi sana yanayouza Pembejeo za Kilimo zikiwemo mbolea,madawa ya kuulia wadudu pamoja na mitambo/machine mbalimbali zinazotumika kufanya kazi za Kilimo.katika picha hapo juu muuzaji mojawapo akiwa anaunganisha aina mojawapo ya kupulizia dawa shambani ili aweze kuifanyia majaribio kabla yakumuuzia Mteja wake. Kumbe Kariakoo ni Soko muhimu sanaa kwa kila mmojawetu ikiwa wewe ni Mlaji au Mzalishaji. Karibu sanaa Kariakoo Soko Kuu upate mahitaji yako.

Monday, May 26, 2014

Soko Kuu la Kariakoo na umri wake wa miaka 40

 Soko Kuu la Kariakoo ambalo linasimamiwa na Shirika la Masoko ya Kariakoo (SMK) tangu mwaka 1974; kwa mujibu wa Sheria Na.36 ya Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.Shirika hili itakapofika tarehe 8/12/1914 litakuwa linatimiza miaka 40 tangu Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius K.Nyerere alipofungua rasmi shughuli za uendeshaji wa Shirika hili hapo tarehe 8/12/1974.
Kila mahali huwa na taratibu zake za kiutendaji katika kusimamia watu,katika picha hapo juu utaona baadhi ya askari wa Shirika wakiwa katika ukaguzi wa mpangilio wa bidhaa ambazo wafanyabiashara hupanga katika maeneo yao tofauti na taratibu za Shirika.Wafanyabiashara hawa wakati mwingine baadhi yao huvuka alama za mistari ambayo imechora kuwaonesha mipaka ya  sehemu zao; hivyo hulazimika maaskari hawa kufanya operesheni ya kukagua maeneo mbalimbali ili kuwarekebisha wale wanaokuwa wamekiuka utaratibu huo wa upangaji bidhaa zao.

Kutoka Sokoni Kariakoo leo!

 Karoti na Pilipili Hoho pamoja na mboga  mbalimbali  za majani hupatikana katika Soko kuu la Kariakoo kwa wingi sana kila siku. Lakini bidha hizi zote zipo katika viwango vya hali ya juu katika ubora kwa mlaji kwa kuzingatia mazingira bora ya Soko la Kariakoo llilopo hapa Jijini Dar es Salaam-Tanzania.
Nyanya kutoka Iringa zinaingia katika Soko Kuu la Kariakoo kila siku katika majira haya. Nyanya hizi kutoka mkoani Iringa huanza msimu wa mwezi Mei na kuendelea; zina ubora wa kipekeee sana katika matumizi.Sasa usikose kujipatia bidhaa hii bora fika Kariakoo Sokoni eneo la Shimoni ambapo utaweza kupata kwa bei ya jumula na rejareja kwa kadiri ya mahitaji yako iwe ya familia au biashara. Karibu sanaaaa!

Thursday, May 8, 2014

Bodi ya Ushauri ya Shirika la Masoko ya Kariakoo ilikutana leo asubuhi

 Mweneyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Shirika la Masoko ya Kariakoo Bwana Wilson Kabwe ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu wa Jiji la Dar Es Salaam akifungua Kikao cha dharula cha Bodi hiyo leo mapema asubuhi. Kikao hicho kilifanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Shirika la Masoko;kikao hicho kililenga kujadili agenda moja tuu muhim ambayo ni Mstakabali wa Shirika la Masoko ya Kariakoo baada ya bomoabomoa iliyofanywa katika maeneo ya Viwanja vya Shirika hilo mwezi mmoja uliopita.
 Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko Bwana Florens Seiya ambaye ni Katibu wa  Bodi hiyo alipokuwa akitoa taarifa ya Shirika kuhusiana  na bomoabomoa  na athari ambazo zimelikumba Shirika pamoja wafanyabiashara ambao walikumbwa kwayo. Pamoja na hasara kadhaa wa kadhaa katika taarifa yake aliyoiwasilisha kwa Bodi hiyo na hatua kadhaa  ambazo Uongozi wa Shirika la Masoko ulizichukua hadi sasa.
 Mwenyekiti wa Bodi Bwana Wilson Kabwe mwenye kitabu chenye rangi nyekundu  katikati akiwa katika kutembelea maeneo ya viwanja vya Shirika mapema leo asubuhi kwani mara baada ya kufungua kikao hicho cha Bodi aliamuru  Wajumbe wa Bodi kwenda site ili kujionea hali halisi na ramani inayoonesha mipaka ya viwanja vya Shirika la Masoko;ili kuwapa picha halisi Wajumbe wakati wa kuchangia mawazo yao.Aliyeshika bahasha ni Meneja Mkuu wa Shirika.
 Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko Bwana Florens Seiya akitoa maelezo kuhusu ramani na mipaka ya viwanja vya Soko Kuu la Kariakoo kwa Wajumbe wa Bodi mapema leo asubuhi.Shirika la Masoko ya Kariakoo lilianzishwa kwa Sheria Namba 36 ya  Bunge ya Mwaka 1974 hivyo lina Haki zote za kuendesha shughuli zake katika viwanja bila kuingiliwa na Taasisi nyingine kama yalivyo Mashirika mengine ya Umma hapa nchini.
 Eneo hili ambalo Wajumbe wamesimama na kupewa maelezo ni barabara ya Pemba ambapo  pembeni yake kuna kisima cha maji ambacho kinamilikiwa na Shirika,ambacho mwezi mmoja uliopita kilkuwa kimevunjwa pampu yake na wakati wa bomoabomoa iliyoendeshwa na Manispaa ya Ilala na katika siku chache baadaye Wahandisi wa Shirika walikifanyia ukarabati.
 Mwenyekiti wa Bodi Bwana Wilson Kabwe akiwa ameongozana na Wajumbe wa Bodi hakuishia tuu maeneo ya nje; bali aliingia hadi maeneo ya Shimoni kujionea hali halisi ya Wafanyabiashara wanavyopata shida kwa msongamano mkubwa ambao umesababishwa na kitendo cha kubomolewa eneo la Soko la Wazi na kuwafanya wafanyabiashara hao kukimbilia wote Shimoni. Hapa akielekea eneo la Gate la kuingilia Shimoni maarufu kama Gate (5).
Hapa ziara  ilikuwa inaendelea kuelekea Shimoni kwenye Soko la Jumula,kutoka  kushoto ni Mkuu wa Kitengo cha Usalama wa Shirika Bwana Jossam Mzava, Bibi Ester Chogero Katibu wa TUICO katika Shirika la Masoko,Mwenyekiti wa Bodi Bwana Wilson Kabwe,Bwana Mwakabinga Meneja Utumishi kutoka Jiji,Meneja Mkuu wa Shirika Bwana Florens Seiya na Bibi Dk.H.Kawawa ambaye ni Bibi Afya wa Jiji la Dar Es Salaam pamoja na wajumbe wengine.

Wednesday, May 7, 2014

Kutoka Soko Kuu la Kariakoo leo!! Shirika la Masoko ya Kariakoo limesaini makubaliano na SIBESONK.

 Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo akisaini Waraka wa makubaliano (MoU) ambao utaiwezesha Kampuni ya SIBESONKE ya nchini Finland kutumia Mfumo wa Taarifa wa Kielektroniki unaomilikiwa na Shirika la Masoko ya Kariakoo katika kuwatumia taarifa za bei za mazao mbalimbali yanayouzwa  katika Soko Kuu la Kariakoo. Kampuni hiyo iliwakilshwa na Mkurugenzi wake Mkuu (CEO) Bwana Uwe Schwarz.
 Bwana Uwe Schwarz akisaini waraka wa makubaliano (MoU) ili Kampuni yake SIBESONKE yenye makao Makuu nchini Finland iweze kutumia Taarifa zinazokusanywa katika Database ya Shirika la Masoko  ili kuwatumia Wakulima,Wafanyabiashara pamoja na Wadau wengine wa bidhaa mbalimbali ambazo huuzwa katika Soko Kuu la Kariakoo lililopo Jijini Dar Es Salaam.
 CEO wa SIBESONKE akisaini MoU katika Ofisi za Shirika la Masoko anaemuelekeza ni Mwanasheria wa Shirika Mrs.Glory Kalabamu na anaeshuhudia ni Bwana Anderson Shaka yeye ni Mkuu wa Kitengo cha ICT katika Shirika la Masoko ya Kariakoo.Utiaji saini huo umefanyika leo mchana katika Ofisi za Shirika.
 Bwana Uwe Schwarz Mkurugenzi Mkuu wa SIBESONKE akiwa Ofisini kwa Meneja Mkuu pichani hayupo mara baada ya kuwasili ili kusaini Makubaliano (MoU);wa kulia kwake ni Mkuu wa Kitengo cha ICT wa Shirika la Masoko Bwana Anderson Shaka.
 Katika picha hapo juu kutoka kulia ni Mkurugenzi Mkuu (CEO)wa kampuni SIBESONKE Bwana Uwe Schwarz kutoka Finland,Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo,Bwana Florens Seiya,Mkuu wa Kitengo cha ICT wa Shirika la Masoko ya Kariakoo Bwana Anderson Shaka na Mrs. Glory Kalabamu Mwanasheria wa Shirika la Masoko;mara baada ya kusaini (MoU) ya kutumia KMC DBS ili kupata taarifa na kuzirusha kwa Wakulima na Wafanyabiashara.Zoezi la utiaji saini lilifanyika leo mchana katika Ofisi za Shirika Jijini DSM.
Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo akipeana mikono na Bwana Uwe  Schwarz (CEO) wa Kampuni ya SIBESONKE mara baada ya kusaini makubaliano ya kupata idhini ya kutumia Mfumo wa taarifa wa Shirika kurusha taarifa za bei za mazao yanayouzwa katika Soko Kuu la Kariakoo.